Jumatano 11 Februari 2026 - 23:30
Matangazo ya kufunguliwa kivuko cha Rafah ni habari za upotoshaji kutoka Israel

Hawza/ Israel imetangaza kuwa imefungua kivuko cha Rafah kwa ajili ya Wapalestina kusafiri, lakini licha ya maombi ya baadhi ya wananchi, uwezekano wa kuvuka haupo, na ni watu 180 tu walioweza kuvuka mpaka tangu tarehe 2 Februari baada ya kupitia mchakato mrefu sana na wenye mateso, na kuelekea Misri.

Kwa mujibu wa Kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, matangazo haya hayajaleta utulivu mkubwa kwa familia zilizo ndani ya Ghaza. Wengi wa wale waliopata ruhusa ya kutoka walikuwa watu waliokuwa katika hali mbaya ya kiafya baada ya kusubiri kwa mda mrefu, na wanahitaji huduma za haraka za matibabu. Hata hivyo, kwa idadi kubwa ya watu, kivuko hiki kimebaki kikiwa kimefungwa kwa vitendo, jambo linalothibitisha kwamba licha ya matangazo ya mara kwa mara kuhusu hatua za “kurahisisha”, mawasiliano ya Ghaza na ulimwengu wa nje bado yamekatika.

Harakati hizi chache za kuvuka, hata kwa kiwango kidogo, hazijakidhi mahitaji. Maelfu ya watu, wakiwemo wagonjwa ambao matibabu yao hayawezekani Ghaza, wamekwama nyuma ya mpaka huo, huku uhaba wa chakula, dawa na huduma za msingi ukiendelea. Wakazi wa Ghaza wanaelezea kwamba matangazo ya kufunguliwa kwa Rafah kuwa ni operesheni ya kiishara, na wanasema hakuna mabadiliko yaliyotokea katika maisha yao ya kila siku chini ya mabomu, njaa na ukosefu wa usalama unaosababishwa na vita na mauaji ya kimbari ya Israel.

Kwa kuwa watu wa Ghaza wanaendelea kulazimika kuvumilia vikwazo na njaa kali, mtiririko mdogo wa kuvuka huko Rafah hauoneshi maendeleo, bali ni ukumbusho wa dhulma endelevu ya utawala wa Kizayuni wenye umwagaji damu dhidi ya nyanja zote za maisha ya raia na watu wa kawaida wa Ghaza. Kwa wengi, faraja ya kweli itapatikana tu kwa kumalizika mzingiro na kusitishwa kwa uharibifu ambao kwa zaidi ya miaka miwili umefafanua maisha ya Ghaza.

Chanzo: SAFA NEWS

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha